Pages

Wednesday, July 12, 2017



JE MUNGU ANAHITAJI SADAKA AU MICHANGO?

MATHAYO 6:1-4

BWANA YESU wa Nazareti asifiwe, kutoka katika kichwa cha somo hili, Je! MUNGU anahitaji sadaka au anahitaji michango au MUNGU hupokea sadaka tu au MUNGU hupokea na michango pia? Jibu tutalipata hapa hapa.

MUNGU anayo njia ya kumbariki mtu na kila unachokitoa kwa hiari yako pasipo kuchangishwa hiyo hupokelewa na MUNGU na anakubariki. Ukisoma Mathayo 6:1 “Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa BABA aliye mbinguni.” Hii ni michango inayofanywa makanisani au unapofanya harambee usitegemee kuwa utapata baraka kwa MUNGU.

MUNGU anataka utoapo iwe ni siri yako wewe na MUNGU sasa unapoagizwa kutoa michango ya kazi ya MUNGU, kumbuka yeye hupenda kazi yake ifanywe na sadaka na siyo kwa michango. Michango ni kwa mambo mengine ya kijamii inaamriwa kabisa, ila MUNGU yeye anajitegemea kwa kupitia sadaka. MUNGU siyo masikini wala sio omba omba hana shida na akitaka kufanya jambo lake anauwezo wa kuamuru kusi na kasi imtolee sadaka. Wapo watu wengi ambao wanalia na kumkumbusha MUNGU sadaka zao kwa kusema, MUNGU kumbuka nilikuchangia pale kanisani, nikumbuke na mimi? Ninachokueleza usimsumbue MUNGU tena, acha kabisa, kwa maana ulipokea thawabu toka kwa wale watu uliowatolea michango, yawezekana wakakusifu ukaona unafaa mbele za MUNGU, kumbe ulifaa mbele za wanadamu wenzako tu uliowachangia na sio mbele za MUNGU.

MICHANGO KWA MAKANISA: (MICHANGO YA MAKANISA NI UGONJWA MKUBWA)


Michango makanisani ni ugonjwa ulioletwa na shetani ukaingia na kuliteka kanisa, kanisa likafuata neno lisilo na pumzi ya MUNGU wakafanya michango ndio sadaka, kumbuka sadaka ambayo MUNGU anahitaji hataki ijulikane halafu wewe unawajulisha watu, unatangaza na unapigiwa makofi na vigelegele na wanadamu, wanakutukuza wewe na kwa njia hii watumishi wengi sana wameachwa na MUNGU kabisa japo wapo baadhi yao ambao walijiita na wengine wameingia katika serikali ya shetani, ya ufalme wa shetani hao hawana hofu wala aibu wa kuubomoa mfumo wa sadaka na hufanya mchango. Hata YESU alipoingia hekaluni alikuta mambo hayo na alileta vurugu kwa kuwa haifai kufanyika katika nyumba ya BABA yake. Je! Ninyi mataifa hamna hofu ya MUNGU? Tazama YESU yeye ana hofu ila wewe unayejiita kwa jina lake hauna hofu! Na Je huoni kuwa ndani yako anakaa roho wa shetani na anasimamia utawala wa shetani uimarike katika dunia hii?

Bwana YESU amenituma mimi Hebron, niwaeleze mataifa yote msitumikishwe na watumishi wa michango popote pale, Yeye siyo masikini, upo ufalme wa mpinga kristo, wenyewe ni maskini na ili kuujenga ni lazima michango ifanyike sasa usishangae kwa sababu mimi YESU nilisema watakuja kwa kutumia jina langu na hata kuwapoteza wateule wa MUNGU, sasa uelewe kuwa wapo wateule wa MUNGU na pia uelewe kuwa wapo wateule wa shetani ambao wao huendeleza kazi ya baba yao  kwa kulitumia jina langu, lakini mtawajua kwa matendo yao ikiwemo michango, japo wapo baadhi yao ambao wao waliiga na hata walipoiga walitekwa na shetani sababu MUNGU ni wa haki, tenda haki upate haki.

Ipo michango ya majimbo, ya matawi, ya kwaya, ya wachungaji, ya kanda, n.k. Nataka mjue kuwa kwa kuchangia huko mlipoteza pesa zenu wala hamkuona baraka yeyote ile, MUNGU hupokea sadaka tu, haijalishi ni ndogo au kubwa na ndipo utakapo barikiwa ila michango ni ujanja wa kuwaibia waumini pesa, kwa sababu kisaikolojia utaona aibu kutoa mchango mdogo mbele za watu wengi, kwa kuwa wanajua mwanadamu anapenda atukuzwe na watu hivyo katika michango atatoa zaidi kwa wanadamu na katika sadaka yake atatoa kidogo kwa MUNGU aliyemuumba, akidhani MUNGU hamshangai, anawapenda wanadamu zaidi, mwanadamu anakuwa mchoyo kwa MUNGU.

Na zaidi mahali kama panafanywa michango na wewe ukatoa sadaka zako ujuavyo ujue kuwa bado umetupa kwa sababu katika madhabahu hiyo nuru na giza vimechanganywa na MUNGU hakai mahali kama hapo, kwa sababu huo ni ujangili. Ukitaka kumtolea MUNGU chochote ufanye kwa siri na kwa furaha, ni siri ndani yako na MUNGU atakubariki. Ila kuhusu mchango sahau kabisa kabisa hapo MUNGU hayupo, hata kwenye redio na TV, utasikia na kuona matangazo eti changia na siyo sadaka, mwenye akili na afahamu hayo yote ni ujangili, asema BWANA MUNGU wa majeshi, yeye anapokea sadaka na siyo michango au harambee.

Michango makanisani ni kero kubwa sana kwa waumini, hata baadhi yao wameacha kwenda kanisani kabisa kwa sababu ya kulazimishwa kutoa pesa kwa njia ya michango kuanzia Januari hadi Desemba; ni wizi mtupu, waumini wanaibiwa pesa zao kwa njia hiyo na wezi wa kiroho, usikubali tena kutoa michango, hata madeni uliyoahidi na unayoendelea kudaiwa usilipe tena na mbinguni utaenda, uokoke uishi maisha matakatifu.

NABII HEBRON.