Pages

Friday, June 23, 2017

JE! MUME AU MKE ANAYEPATIKANA KWA NJIA YA UCHAWI NA NDOA HIYO KUFUNGWA KANISANI, JE NI MUNGU NDIYE ANAWAUNGANISHA WAWE MWILI MMOJA?

Bwana YESU asifiwe! Watoto wote wa MUNGU, napenda mjue kuwa Mwenyezi MUNGU ana mpango mzuri kwa ajili ya kila mmoja ila umefika wakati wake wa kuwafundisha wanandoa wapate kuwa mwili mmoja kwa kusudi lake. Lipo tatizo kwa baadhi ya watu, wanazidi kumkosea MUNGU wengine kwa kujua na wengine bila kujua. Wengine wanaamua kwenda kutafuta mke au mume wa kuoa kwenye malango ya kuzimu, yaani wachawi. Watu hawa wakisha fanikisha kumloga mwenzake ili awe mke au mume wake, kisha wanakwenda kanisani kufunga ndoa, wakifikiri kuwa MUNGU atawaunganisha wawe mwili mmoja kama mke na mume na atatambua kuwa ni ndoa takatifu na kumbe hiyo ni ndoa ya giza (nyeusi).

 Napenda muelewe kuwa watu wengi wanateseka na wengine wanafikiria kwenda kwa waganga ili wapate wenzi wao,  nawaeleza hata kama mtu atafanikiwa kumloga mwenzake, bado MUNGU hata itambua ndoa hiyo, haijalishi anayefungisha ndoa hiyo ni mtumishi wa aina gani, ila mwenye macho ya rohoni ataomba na ataona hapo hapo tatizo na uchumba utasambaratika, ila ikiwa mtumishi hana macho ya  rohoni atakua amedanganywa na atafungisha ndoa kwa akili yake na ibada ikafanyika, ila kwa MUNGU ibada hiyo ni uchafu mbele zake, kwa sababu siri imefichwa machoni mwa wanadamu ila MUNGU yeye hafichiki, ndoa hiyo itakuwa imeunganishwa na shetani kwa sababu asili yake ilianzia kwa wachawi, wakatuma majini ya kike na ya kiume ndani yao wakakubaliana kupitia nguvu  za majini na majini hayo ndiyo yaliyofanikisha. Sasa kwa nini umshirikishe Mwenyezi MUNGU ushetani? Hapo utakua umeelewa, kama uliyatenda hayo, unayo dhambi   ikiwemo ya kudhulumu haki ya mwenzako ya ndoa ya mpango aliyopangiwa na MUNGU, na kati ya wanandoa mmoja wenu ambaye amemdhulumu mwenzake haki hiyo na kisha unampatanisha na haki ya shetani uliyoipanga kichawi, tambua kwamba umebeba dhambi hiyo.

Hata ukisoma Biblia, Waebrania 13:14, imeandikwa ndoa na iheshimiwe na watu wote, hapa tayari agizo la MUNGU litakuwa limedharauliwa. Nafundisha ili wengi wapate kujua kuacha kupenda kutafuta wake/waume kwa wachawi, waje kwa YESU kwa sababu hata ukimpata mke au mume kwa njia ya kichawi na ukafunga ndoa kanisani au kuibariki bado haiwezekani MUNGU kuitambui milele kwa sababu hapana ushiriikiano kati ya giza na nuru. Kwa hiyo ndoa inakuwa ya shetani na majini siku zote labda mpaka neema ya MUNGU imkute aliyedhulumiwa na kumtoa hapo.

Hata wale wenye miaka 50 katika ndoa, endapo walitumia uchawi, hata iwe ni mwezi mmoja au mwaka mmoja bado nataka uelewe kuwa MUNGU haitambui ndoa hiyo kabisa, hata kama mtaishi milele mpaka kufa, bado hautakuwa na ndoa inayotambulika mbele za MUNGU, bali utakuwa na ndoa inayotambulika mbele ya shetani. Hivyo basi watoto wa MUNGU kwa kuyajua hayo yote msipende kutafuta mke au mume kwa njia hizo, hata kama utatumia mamilioni ya gharama za harusi kubwa bado itakuwa sio harusi inayotambulika mbele ya MUNGU na pia bado mtakuwa ni wazinzi milele kwa sababu chanzo cha ndoa hiyo sio MUNGU.  Katika ndoa hiyo ni vigumu kuelewa ni nani aliye enda kwa mganga ndipo akampata mwenzake, kwa sababu endapo ni kijana hatasema na endapo ni binti hataweza kumweleza mwenzake kwa kuogopa kuachwa au kutokuaminiwa na kama ikitokea kutoa siri hii ni mara chache sana, ila kumbuka MUNGU anaona kila kitu.

Penda kumtegemea Mwenyezi MUNGU katika kila jambo, na yeye atakufundisha, yeye ni MUNGU wa mafanikio yako na usitegemee tena malango ya kuzimu na waganga wakienyeji, wachawi, wasoma dua, wasoma nyota, ramli na zaidi kila mtu amshike YESU na kuishi maisha matakatifu, hao waganga na wachawi hawatakuweza kwa Jina la YESU.

Tubu, sema, BWANA YESU, naomba unisamehe dhambi zangu zote, sitashiriki kutafuta mume au mke kwa njia ya kichawi na sitaki dhambi tena, naomba uandike jina langu katika Kitabu chako cha uzima wa milele. Alichokiunganisha MUNGU ni cha MUNGU na alichokiunganisha shetani ni cha shetani.

Angalizo: Usije ukamlazimisha MUNGU kupokea kazi za shetani ili azikubali kwa sababu MUNGU na shetani hawana uhusiano. Shetani na wafuasi wake ni maadui wa MUNGU na hawana ushirika wowote. Natumaini watu wengi wamepona na wataacha kwenda kwa wachawi, ukifanya hivyo ujue kuwa utakuwa wa shetani, hii ni sawa na kutafuta mtoto kwa mganga wa kienyeji halafu ukizidiwa  unamleta kwa MUNGU ili ampokee (kuwekwa wakfu). Mtoto huyo hatapokelewa na MUNGU, kwa sababu atakuwa amepatikana kupitia malango ya kuzimu, na mwisho mtoto huyo atakuwa na maisha ya ajabu ajabu na hatafanikiwa mapema, hataishi maisha marefu na baada ya muda mfupi shetani atachukua mtoto wake. Wengi nikiwaombea naona baadhi yao wamepatikana kwa njia hizo na MUNGU hawapokei kama watoto wake, mbingu inakua imenyamaza kimya.

NABII HEBRON.