Pages

Saturday, November 22, 2014

ADAMU WA PILI NI YESU WA NAZARETI WALA SIYO MWANADAMU YEYOTE YULE. 
(1 WAKORINTHO 15: 45-49).

BWANA YESU ASIFIWE watu wote wa mataifa yote, wakristo, wapagani na wengineo wote mlioumbwa kama wanadamu, nawasalimu kwa jina la mwana wa MUNGU wa pekee ambaye ndiye YESU WA NAZARETI aliyekuja duniani akafanyika kuwa yeye ndiye Adamu wa pili. Nitaelezea kwanza kwa nini YESU anaitwa ndiye Adamu wa pili? Hii ni sababu MUNGU alikwisha muumba mwanadamu wa kwanza na akampa jina Adamu huyu ndiye Adamu wa kwanza na ambaye kupitia yeye tunaitwa wanadamu kwa heshima ya jina lake na kama ndiye mtu wa kwanza kuumbwa na mwenyezi MUNGU, baada ya Adamu wa kwanza kuanguka katika bustani ya Edeni akiwemo na mke wake Eva soma katika kitabu cha Mwanzo 3 yote. 

Hivyo basi haikuwezekana tena binadamu ajikomboe tena kutoka katika mikono ya shetani. Ikabidi sasa MUNGU amlete mtu wa mbinguni mwenye nafsi yake akiwa na sura ya mbinguni ili aje aukomboe ulimwengu akazaliwa kwa kupitia Mama Maria ndiye aliyeibeba hii mimba kwa uwezo wa ROHO MTAKATIFU bila ya kubeba uja uzito wa mwanadamu, ndiyo sababu YESU anaitwa Adamu wa pili sababu yeye alitoka mbinguni na ndio sababu Mama Maria hata ukisoma biblia utaona mchumba wake Yusuph akimkuta tayari ana mimba japo ni bikira ila akaeleweshwa na MUNGU kupitia ndoto akaelewa.

YAFUATAYO NI MANENO KUTOKA KATIKA BIBLIA YANAYOHAKIKISHA YESU NDIYE ADAMU WA PILI NA SIYO BINADAMU MWINGINE.

a)    Daniel 7: 13-14: nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa usiku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.

Sasa hapa unaona unabii ambao ulioandikwa kuhusu mwanadamu atokaye mbinguni na akaja ambaye yeye ndiye aliyepewa mamlaka yote ya kutawala mataifa yote ni kwa lugha zote na mamlaka yake ni ya milele. Sasa huyu ndiye Adamu wa pili, sasa cha ajabu wametokea waongo wanaomkufuru MUNGU kwa kuchukua utukufu wa YESU na kujiita Adamu wa pili, sasa jamani hauoni huu ni ushetani wa kumchokoza YESU wa kulipindua neno lake? Je anayejiita Adamu wa pili yeye ndiye anayetawala mataifa yote zaidi kushinda YESU? Jibu, siyo. Swali lingine je biblia imetuagiza tutumie jina lipi? Jibu ni YESU WA NAZARETI. Sasa mpaka hapo uelewe ni dhambi na ni ushetani kuingilia cheo cha YESU au kujiita wewe ni YESU.

b)    1 Wakorintho 15: 45- 49- ndivyo ilivyoandikwa, mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyohai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha. Lakini hautangulii ule wa roho, bali ule wa asili; baadaye huja ule wa roho. Mtu wa kwanza atoka katika nchi, ni wa udongo. Mtu wa pili hutoka mbinguni. Kama alivyo yeye wa udongo, ndivyo walivyo walio wa udongo; na kama alivyo yeye wa mbinguni, ndivyo walivyo walio wa mbinguni. Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo, kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni.
Hapa ni mistari ambayo inakuhakikishia kuwa YESU ndiye Adamu wa pili. Adamu wa pili ametoka mbinguni ambaye ndiye YESU alitoka mbinguni akazaliwa kwa sura ya mwana wa Adamu, ndiye sababu anaitwa Adamu wa pili na ilitabiriwa akatokea na akaja hapa ulimwenguni akaifanya kazi yake akaimaliza akarudi mbinguni. Sasa hivi tunasubiri aje katika unyakuo kulinyakua kanisa.

Mpaka hapa umeshapata picha ya ukweli kuwa YESU ndiye Adamu wa pili sababu nimekula sifa za kweli za Adamu wa kweli ambaye ndiye YESU WA NAZARETI na hata katika ulimwengu wote hakuna jina lenye nguvu na mamlaka kama la YESU WA NAZARETI.

Swali je binadamu akijiita yeye ni Adamu wa pili je hauoni huyu anavuruga mpango wa MUNGU ili kuwapoteza watu waende Jehanamu kama wenyewe watakavyo kwenda na wengine tayari wamesha kwenda kusubiri hukumu ya moto? Kila bara watumishi wa ajabu ajabu wametokea ili kuwapoteza hata wale wateule.

Kila mtu unayoisoma biblia na unayo akili timamu kama haujatekwa na shetani au fikra zako kufungwa lazima utakubaliana na mimi Nabii Hebron kuhusu kuwa hakuna Adamu wa pili tena zaidi ya YESU. Kama atatokea ajiite hivyo au alishatokea muelewe huyo ni muwongo na ni adui wa MUNGU na pia amechukua utukufu wa MUNGU na kumpinga YESU yeye hajui lolote, au kwa maana nyingine, niulize swali sababu umeshajua Adamu wa kwanza alitokana na mavumbi na Adamu wa pili 1 Korintho 15: 47 alitoka mbinguni, sasa hivi inaingia katika akili yako mtu amezaliwa hapa duniani, ametenda dhambi, wala hajatabiriwa kuwa yeye kwa jina lake ataumiliki ulimwengu kama YESU? Sasa hauoni wanaojiita hivyo ni waongo? Na unapokuwa chini yao ina maana unatawaliwa na wao na siyo YESU wala MUNGU sababu MUNGU hajapanga hivyo ila shetani ili awateke watu fahamu na awamiliki anawatumia wale watumishi ambao yamkini YESU aliwaita hapo mwanzoni na wengine wamejiita wakamsaliti yeye sasa shetani anawatumia hao hao ili kuwapoteza wanadamu kama ilivyo sasa. Hii ni dalili tosha uelewe watumishi walivyomsaliti YESU mpaka shetani akateka kama 98% ya watu wote wa ulimwengu huu.

Jambo lingine niwaulize swali je YESU hakuimaliza kazi yake hapa ulimwenguni? Jibu, alimaliza. Sasa wengine wanakuja kuwadanganya watoto wa MUNGU eti YESU hakuifanya kazi yote aliyotumwa? Je inakuingia katika akili yako? Wanaosema YESU hakumaliza kazi yake aliyotumwa na MUNGU hao ni waongo na ndani yao ni Lusifa anaongea siyo roho wa MUNGU.
Yohana 1:1, 14, Mathayo 11:9-14 SOMA.

NOTE:
Mimi kama mimi Nabii Hebron, nawasihi watu wote huu ni wakati mbaya na wa hatari sana YESU ambaye ndiye Adamu wa pili, muda wowote atarudi kulinyakua kanisa lake ila siku na muda hiyo sijui. Utaulizwa wewe je uliliteteaje jina lake pale lilipochafuliwa? Au kama unampenda kweli YESU kwa nini usiwaeleze watu ukweli wasidanganyike pale ambapo hata wanadamu wanajifananisha na yeye wakati tunajua hakuna zaidi ya YESU aliyetoka mbinguni akawa binadamu? Akaishi na wanadamu kisha akapaa na atakuja kulinyakua kanisa lake!
Na siku moja nilikuwa naongea na YESU 2013 akaniambia Hebron, hivi mwanadamu ni nani mpaka ajifananishe na MUNGU? Kama YESU mwenyewe anachukia pia na Malaika wanachukia, je ni nani ajiite yeye ni MUNGU wa majeshi? Sasa kama yeye ni MUNGU wa majeshi na anaonekana kwa macho ya wanadamu basi kila mtu angekufa sababu imeandikwa hauwezi ukamuona MUNGU halafu ukaishi. Sasa kama tunaishi au unaishi na umemuona mtu anajiita yeye ni MUNGU wa majeshi basi hiyo ni picha halisi yeye ni adui wa MUNGU kama vile shetani alivyotaka kuuchukua utukufu wa MUNGU akatupwa kuzimu na ndivyo njia ni moja na hata atakayemuamini mtu wa jinsi hiyo na yeye atafuata njia hiyo hiyo. Tazama hata shetani alipofukuzwa mbinguni alifukuzwa na wafuasi wake ambao ndio malaika waliomuasi MUNGU. Najua hata sasa watu wanatengenezewa njia ya kumuasi MUNGU ili wachomwe moto na wao hawajui wanatekwa fahamu na akili zao.

Sasa mfunguke fahamu na akili watu wote wa mataifa yote msiamini kabisa mtu yeyote awe ni Nabii, Mtume, Mchungaji, Mwinjilisti au kiumbe chochote kile. Kitakachojiita chenyewe ndio Adamu wa pili, anayo mapepo siyo ROHO MTAKATIFU 100% wala hapeleki mtu kwa YESU bali ni kwa shetani. Adamu wa pili ni YESU WA NAZARETI ndiye tuliyopewa zawadi na MUNGU ili kupitia yeye ndio njia atufikishe mbinguni na atulinde! Sasa iweje wengine katika nchi mbali mbali wajiite wao ni Adamu wa pili? Je inakuingia katika akili yako? Nawasihii kama unapenda usiende Jehanamu epuka na watu wote wanaojiita wao ni YESU au MUNGU wa majeshi au ROHO MTAKATIFU. Hao ni wapinga Kristo.

Jambo lingine Adamu wa pili anaishi milele na ndiye atakayekuja kuuhukumu ulimwengu na ndiye atakayekuja kulinyakua kanisa ambaye ndiye YESU WA NAZARETI. Sasa swali je hawa wanaojiita Adamu wa pili ndio watakao uhukumu ulimwengu?? Jibu siyo na je wanaishi mbinguni kama YESU au wapo hapa hapa tu kama wewe? Na pia niulize swali, je YESU anafananishwa na mtu yeyote? Jibu hakuna. Watoto wa MUNGU ulimwengu umemgeukia shetani, sasa mnaomjua YESU wa kweli mpinge kwa nguvu watu wanaobadilisha biblia na pia akatokea mtu mwingine ajiite yeye ndiyo Adamu wa kwanza, nawatangazia hao ni mapepo kutoka kuzimu kwenye asili ya baba yao wa uongo. Akitokea mtu anajiita yeye ndiye Adamu wa kwanza elewa yeye ni muwongo na ni adui wa MUNGU. Akitokea ajiite yeye ni Adamu wa pili mjue yeye ni adui wa YESU 100%.

Sema BWANA YESU naomba unisamehe dhambi zangu, unitoe katika mikono ya watumishi wa jinsi hii ili nisiangamie. Uniandike jina langu upya katika kitabu chako cha uzima wa milele, najitenga nao kiroho na kimwili najikabidhi kwako wewe uliye Adamu wa pili kutoka mbinguni ambaye ndiye YESU WA NAZARETI. Uniongoze, unilinde, mi simtaki shetani tena, nimetambua kwamba nilikuwa katika upande wa adui yako. Amen.


NABII HEBRON.