Pages

Thursday, August 2, 2018


JINSI YA KUJUA MCHUNGAJI ANAYEONGOZWA NA ROHO WA UONGO
NA SIYO ROHO WA MBINGUNI

Shalom watu wote wa MUNGU wa mataifa yote, hiki ni kipindi cha mwisho ambacho tunamsubiria YESU aje kulinyakua kanisa, yaani yeye aliyeokoka na kuishi katika maisha matakatifu ndiye atakayechukuliwa, kwa sababu ndivyo alivyosema hata katika Neno lake, na Neno lake ni kweli, hasemi uongo na wala siyo kigeugeu na habadiliki bado atabakia kuwa MUNGU katika nafasi yake ile ile. YESU mwenyewe amesema bayana, angalieni watakuja wakitumia jina langu, watawadanganya wengi wakitumia jina langu. Hao ambao YESU anawataja watawadanganya watu wengi ni wachungaji au wanaoitwa au wanaojiita kwa jina la YESU, baadhi yao ni waongo ila imekuwa ni vigumu kwa mataifa kuelewa huu uongo.

Nitaelezea kuhusu uongo wa kutumia Biblia ambacho ni Kitabu Kitakatifu na jinsi ambavyo watumishi hao ambao ni waongo ambapo aidha kwa kutumia nafasi zao au madhabahu zao, wanapoamua kuchanganya ukweli na uongo katika huduma za kiroho wanazozifanya. Kwanza nataka muelewe kwamba MUNGU yeye siyo mwongo, yeye ni mkweli muda wote, bali shetani yeye ndiye mtengenezaji wa roho za uongo au nguvu za uongo. Na pia kila mtu aelewe kwamba huyu YESU jina lake ni zuri sana na mtu akilitaja huwa anaaminika ni mtu safi, sasa wapo waongo wanaolitumia jina hili pasipo watu kujua Biblia inasema nini juu ya haki zao kutoka kwa MUNGU, hudanganywa na wachungaji waongo. Nasema waongo kwa sababu mchungaji utamjua kwa matendo yake anayoyafanya au injili anayoifundisha, je ni kweli tupu anayofundisha au anachomekea na uongo ili aibie watu mali zao au awapeleke watu jehanamu! Mchungaji akiwa kipofu hata wewe muumini utakuwa kipofu, labda Neema ya MUNGU ikusaidie utoke kwenye upofu huo. Ukijua ukweli kama mchungaji au mtumishi anafundisha uongo na ukamweleza atachukia kwa sababu umejua kwamba yeye ni kipofu, sasa badala ya yeye kukubali na kuacha uongo atakuchukia kwa sababu yule roho wa ibilisi aliyopo ndani yake atajua umemjua na hivyo hakupati tena.

Nitaelezea mifano michache ambayo baadhi ya watumishi wanasema uongo na wamejawa na roho wa shetani, na kama wamejawa na roho ya uongo basi wanaongozwa na shetani. Wapo wanaojijua na wengine hawajijui na ndipo ile siku ya mwisho YESU anasema watalia na kusaga meno, naye YESU atasema sikujui sikujui. Je wewe umeshafikiria ni kina nani hao? Baadhi yao ni watumishi na wengine wanao fanana na hao. Mfano, MUNGU anasema muwaombee watu na msiwatoze watu pesa za maombezi, sasa anapotoza watu pesa na kusema eti MUNGU anawaagiza watoe kiasi Fulani, Je hapo hamuoni huo ni uongo mkubwa uliokithiri na watu hawalijui hilo! Baadhi wanaziita hizi tozo (charges) sadaka na watu pasipokujua wanaamini na kumbe unaibiwa na hautapata baraka yeyote toka kwa MUNGU, bali utaendelea kufilisika na kuangamia wakati huyo mtumishi akiendelea kufaidi matunda ya unyang’anyi na mwisho atatupwa jehanamu. Huo ndio ukweli YESU ameniambia kila anayesema uongo kuhusu Yeye tofauti na Neno basi mwisho wake ni jehanamu, hata mimi Hebron tokea aniite aliniambia usije ukamtoza mtu pesa ndipo umwombee, ukifanya hivyo utachomwa moto. Nawaeleza watumishi msiojua hilo na mkaiga wale waliojiunga na muovu, msipo acha sasa, mtachomwa moto jehanamu, na kila anayetoza watu pesa ajijue anayo ticket ya Jehanamu mkononi mwake, kwanza yeye ni mwizi anawazuia wengine wasiende mbinguni, yaani ukiongozwa na mtumishi anayewatoza watu pesa uelewe anakuambukiza na wewe roho ya kukuzuia kwenda mbinguni kwa sababu yeye haendi. Jinsi alivyo mtumishi na ndivyo alivyo na kondoo, soma Mathayo 23:13.

Jambo jingine ambalo liko wazi kabisa, YESU alisema kila anayetaka kupona na jehanamu ni lazima aokoke sasa iweje baadhi ya watumishi katika dunia hii wanawazuia watu wasiokoke bali wajiite wakristo tu bila wokovu, sasa kama una masikio na usikie, hawa hawaendi mbinguni kabisa na wanawazuia watu wasiokoke ili nao wasiende mbinguni. Ona basi, wao hawataki kwenda halafu wanawazuia na wengine wasiende. Sasa muelewe watu mnaotaka kwenda mbinguni, wokovu ndiyo ticket yako ya kwenda mbinguni na kama haujaokoka uelewe unayo ticket ya kwenda jehanamu. Hapo unafungiwa katika gereza la shetani, unapigwa upofu ili uone upo salama kumbe tayari umekufa kiroho. YESU anarudi, maneno haya usiyadharau, okoka sasa achana na waongo wanaokuzuia usionane na MUNGU aliyekuumba, yeye anakuhitaji, mkatae mpinga kristo na uongo wake. Hata kama mtumishi ameokoka halafu anawatoza watu pesa bado na yeye ni adui wa MUNGU na shetani ndiye rafiki yake. Dunia, huu ni wakati wa kila mtu kujua ukweli ili apone roho yake na ndoto zake zije kutimia, kuwa siku moja ataenda mbinguni na atafika, badala ya kwenda jehanamu.

YESU alibatizwa kwenye mto, Yohana alifanya kama alivyotumwa na MUNGU, sasa nauliza mataifa yote ni nabii gani alitumwa kutoka mbinguni tuje kubatizwa na maji ya kikombe, au maji ya kisima au kubatizwa kwa bendera au kwa jina la mchungaji au kwa vumbi au kubatizwa kwenye beseni? Jibu hakuna, je kama katika Biblia hakuna sasa huoni hiki ni kipimo cha wazi kuona jinsi uongo ulivyopokelewa na upo juu ya vichwa vya mamilioni ya watu wakifikiria ndiyo agizo la MUNGU kumbe siyo na kama siyo basi ni uongo. Watu hawajabatizwa kwa mpango wa kweli wa MUNGU aliyeumba mbingu na nchi, hivyo yeye hana uhalali na wewe kwa sababu umepokea kiapo cha mungu asiyejulikana na kukufanya ubakie kwa huyo asiyejulikana yaani shetani pasipokujua au kwa kujua. Basi ili mpone mataifa yote ni lazima uokoke, hakuna njia nyingine zaidi ya hiyo, hizo nyingine zote ni za uongo na zitakuangamiza. Ninapoandika ujumbe huu nasikia sauti ya YESU ikinieleza haya niyaandikayo kwako wewe kwa taifa lako na kwa sura yako.  Wokovu ni lazima kama unataka kwenda mbinguni na ubatizwe kama Yeye YESU na siyo tofauti. MUNGU habadiliki (soma Ufunuo 22: 18-19). Badilikeni sasa mataifa, okokeni, YESU anawapenda, anajua watu wamedanganywa sana na wanampenda ila hawajui ukweli kuhusu YESU anavyotaka.

Imeandikwa, kanisani ni mahali patakatifu sasa cha ajabu kwa baadhi ni sehemu ya masoko, na pia hata sadaka za fungu la kumi la mazao ya watu imefanywa ni siku ya sherehe, basi wafanye na siku za sherehe za mishahara wawapige watu upofu na cha kusikitisha zaidi siku za sherehe ya mazao wanakuja madalali kufanya mnada katika nyumba ya sala wakitumia jina la YESU, huku ni kumchafua YESU, kumdharau MUNGU na Yeye hakai na watu wa jinsi hiyo.
Zaidi endelea kusoma makala za Nabii Hebron, utajifunza mengi na utawekwa huru, ila WOKOVU ni LAZIMA. Tubu sasa, sema, BWANA YESU naomba unisamehe dhambi zangu zote, unisamehe kufuata uongo kwa kujua au kutokujua, sitaki tena kushiriki dhambi, uandike jina langu katika kitabu chako cha uzima wa milele. Amen.
NABII HEBRON WISLON KISAMO.