Pages

Monday, May 7, 2018


 INJILI ZA MAPOKEO YA WANADAMU ZINAWAPELEKA WATU JEHANAMU
BWANA YESU WA NAZARETI ASIFIWE! Katika makala hii nitaelezea zaidi kuhusu mapokeo ya wanadamu yalivyo na madhara kwa mkristo au mtu yeyote yule unayeyakubali au unayeyafuata ili kumtafuta MUNGU.

Mathayo 15: 5-9 5Bali ninyi husema, Atakayemwambia babaye au mamaye, chochote kikupasacho kusaidiwa na mimi ni wakfu, 6basi asimheshimu baba yake au mama yake. Mkalitangua neno la MUNGU kwa ajili ya mapokeo yenu 7Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, 8watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami, 9Nao waniabudu bure, Wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu”.

Katika neno hili alilolitamka YESU, ‘Enyi wanafiki”! Sasa jiulize ni nani anayeitwa mnafiki na YESU? Mnafiki ni mkristo asiyeyafuata yale aliyoleta MUNGU, huyu ndiye mnafiki anayesemwa na YESU, sasa wewe jipime, utajijua kwa matendo yako, je wewe ni mnafiki au la!!

NINI MAANA YA MAPOKEO YA WANADAMU?
Mapokeo ni kitu ambacho sicho halisi bali ni kitu cha kuchomekewa au kuunganishwa na neno ambalo silo linalostahili ambalo neno hilo linakuwa limeletwa na wanadamu na siyo MUNGU, utajiuliza kivipi? Kila mtu anajua Biblia ni kitabu kitakatifu na kitabu hiki amekileta MUNGU, nikimaanisha yale yote yaliyomo ndani ni Yeye MUNGU kaleta ili wanadamu tuyafuate na zaidi akasema katika kitabu cha Ufunuo 22: 18-19, kisiongezwe chochote wala kupunguzwa. Sasa basi ikiwa mkristo ataongezewa mambo ambayo hakuyaagiza Mwenyezi MUNGU basi hapo mtu huyo atakuwa ameleta mapokeo ya wanadamu na mtu yule ambaye atayafuata na yeye atakuwa sasa anawafuata wanadamu na siyo MUNGU, na jambo hili watu wengi hawalifahamu na linawafanya kibiblia kuwa wanafiki kwa YESU pasipokujua na wengine wakijua kabisa ni wanafiki wenye roho ngumu wasiosikia na kutubu na kuachana nayo.

Swali, kwa nini YESU anasema mnaofuata mafundisho ya wanadamu mnaniabudu bure, hili neno lina maana kubwa sana na mimi Nabii wake nataka nikufunulie hili neno. Ina maana kwamba haijalishi unajiita ni mkristo au umeokoka au unafunga au ni mtumishi, mfano ni mchungaji, lakini pasipo kuachana na kazi unayofanya au unachokiabudu, hata sadaka unazozitoa bado YESU hakuhitaji anakuona wewe ni mnafiki kwake. Sasa ni bora uelewe ili upone na unafiki uliokuwa haujui ukutoke kabisa.

Kwa wewe ambaye utaguswa na mafundisho haya ya Nabii Hebron kwa jinsi alivyonifunulia neno hili takatifu ili ulimwengu upone na usiangamie. Swali jingine la kujiuliza ni kwa nini mapokeo yameletwa na kuchanganywa na neno la MUNGU? Kama mnavyojua YESU yeye ndie chakula cha uzima na mtu atakapolila neno lake atakuwa na uzima, hivyo basi kila mtu anayetaka uzima ni lazima roho yake ipate neno lake kama lilivyo, MUNGU amelihakikisha ndilo linalofaa kwa wanadamu. Sasa shetani na yeye ili aliharibu neno lile ambalo mtu akilila atapata uzima shetani akaleta maneno yake akampa mwanadamu au baadhi ya wanadamu ambao ni waalimu, wachungaji, mitume, manabii, na wengineo, wale ambao hawakusimama imara katika kweli au wale ambao shetani amewazaa kiroho wafanye kazi ya mpinga kristo au wale ambao mwanzoni waliitwa na MUNGU ila baadaye wakamwasi MUNGU wakaingia upande wa mpinga kristo. Sasa unavyoyapokea na kuyaamini hayo mapokeo ya wanadamu na wewe tayari katika ulimwengu wa roho umekuwa mwana wa wanadamu badala ya mwana wa MUNGU, kwa sababu umepokea katika moyo wako ukafanyika uwe mnafiki kwa YESU na kwa MUNGU pasipokujua au kupenda ukayaamini maneno hayo mkayafanya ndio njia yako ya kiroho, na unapoyafuata basi na roho yako ndipo ilipo. Hivyo basi, nimendika ujumbe huu kwa mataifa yote ili ueleweke, kwa sababu YESU anarudi na watu wengi wapo katika mapokeo pasipo kujua na wanarithishwa na kuwafanya baadhi kuwa wanafiki mbele za MUNGU wakati wao wanampenda YESU kikweli ila wametegwa na mtego huu wa mapokeo ya injili ya uongo.

Nitaeleza baadhi ya mapokeo ya kibinadamu na zaidi hata baadhi ya vyuo vikuu vya injili vimeacha neno la kweli na wanafundisha kwa kuchanganya na uongo. Ninaposema uongo nataka uelewe ni jambo lolote ambalo neno halijaagiza lifanywe au mafundisho yanapokuwa ni tofauti na YESU alivyosema katika kitabu chake, yaani Biblia. Sasa cha ajabu katika Katiba hii ya MUNGU alivyowapa wanadamu, wametokea waongo katika baadhi ya imani za kikristo wakabadilisha vipengele kama neno lilivyosema ikawa ni tofauti.

MIFANO:
1.     Ubatizo wa kikombe, ubatizo wa kisima, kubatizwa kwenye tenki, kubatizwa kwa kutumia bendera au kubatizwa kwa jina la mchungaji. Katika Katiba ya MUNGU hakuna batizo za jinsi hii japo hata mimi niliwekewa ubatizo wa kikombe hapo awali ila namshukuru YESU nimebatizwa tena na ubatizo mtakatifu wa maji mengi yanayotembea na hata hao waliobatizwa hivyo siyo kwamba hawampendi YESU bali hawajui ukweli wa neno lilivyo! Kitu cha kujiuliza, ubatizo wa Yohana umetokea wapi? Jibu ni Mbinguni, jiulize sasa ubatizo wa kikombe, kisima na hizo nyinginezo zimetokea wapi? Jibu kwa mwanadamu basi kama umepokea na kuamini ubatizo wa wanadamu na wewe utakuwa mfuasi wa wanafiki ambao YESU amewasema kwa sababu alipo YESU hamtaenda kabisa, kwa sababu mmepokea kiapo cha kibinadamu cha ubatizo halafu kikachanganywa na Neno la MUNGU, yaani YESU akatajwa, Roho Mtakatifu atajwa na mengineyo, hapo bado ni unafiki. Shetani anao uhalali kabisa na wewe kwa sababu mmepindisha, umekubali kufuata ya wanadamu badala ya YESU. Kwa kila mtu afuataye hayo hiyo ni dhambi inatembea na yeye.

2.     Mifano mingine imeandikwa, ukiombea watu usiwatoze pesa, lakini hili ni tatizo na kero kubwa katika ulimwengu wote, hili pokeo la shetani linawatesa sana watu wakifikiri ni Neno la MUNGU kumbe ni neno la pepo kabisa, ambalo linatumika kuwaibia wakristo na wasio wakristo katika sehemu za ibada. Nataka uelewe mambo haya kama alivyonieleza YESU haijalishi utachukia au utafurahi, nimetumwa kueleza ukweli wa Neno lilivyo na kuliondoa giza ili wale wanaopenda kwenda mbinguni waende, wasipelekwe jehanamu. Kila mtumishi anayewatoza watu pesa kwa ajili ya maombi, yeye anakuwa ni mnafiki kwa YESU, na wala hawampendi YESU, na wala hawamheshimu. Ibada hizo zote ni za kinafiki mbele za MUNGU, na zaidi unaposali hapo wewe muumini unaambukizwa kidogo kidogo roho ya kinafiki na hiyo roho ikiingia ndani yako unaanza kupinga kweli ya Neno na mwisho wake unakufa kiroho na hata kimwili. Ukifa kiroho huendi mbinguni kwa sababu shetani anakuwa anao uhalali kwa sababu haukumwabudu MUNGU ulipokuwa hai. Ila mtashangaa, hao watumishi wanaotoza watu pesa wao wanaendelea kufanikiwa, hili lisikushangaze kwa sababu hao hawaendi mbinguni wakifa bali wanaenda moja kwa moja kwa baba yao wa uongo ambaye ni shetani.

Mapokeo ya wanadamu yapo mengi ila nitaelezea machache ambayo ni sugu na utaelewa vizuri kwa mifano. Imeandikwa usiabudu sanamu, lakini sanamu zinaabudiwa, ibada za kumbukumbu za wafu, wakati MUNGU yeye siyo wa wafu. Kumwomba mtumishi akusamehe dhambi zako na ukaungama kwake badala ya kuungama kwa YESU anayesamehe dhambi. Harambee makanisani, wakati YESU alikataa, sasa kanisa limekuwa ni soko, hata hao waliokubali kufanya harambee wakitumia jina la YESU, hao wanakuwa ni wanafiki, kwa sababu YESU hataki unafiki, yeye alimpenda BABA yake na Neno lake. Soma Marko 11:15-18, sasa iweje nyie wanadamu wa leo hufanya kinyume na aliyekuumba? Hivi mnafikiri MUNGU hawaoni? Nawaeleza na hii siyo siri, MUNGU anawaona na mwisho mtapata fimbo yake. Hivyo wacha usije ukachomwa moto, tubu na uokoke sasa hivi. Haijalishi unakesha miaka yote ya ukristo lakini kama unayafuata mapokeo ya wanadamu, YESU anakuona ni mnafiki tu ukimwabudu yeye bure. Je ni wangapi wanamwabudu bure na wangapi wanaendelea kumwabudu YESU bure.

Ukristo wa mapokeo ni kama vile mtu anayefanya kazi na asipate faida yoyote bali ni hasara tupu, au ni sawa na mtu anayelima shamba heka kwa maheka lakini hapati mazao, anavuna hewa tu. Na ukumbuke, hata mkulima huyo atatumia gharama nyingi katika shamba hilo na zitapotelea chini, ndivyo ilivyo na kwa mkristo wenye kufuata mapokeo. Ili upone, ukoka na wala usishiriki katika nyumba zao za ibada za mapokeo, ndio sababu imeandikwa tokeni mkatengwe nao. Wewe unayekaza shingo tii neno hili, ni sauti ya MUNGU kwako na siyo sauti ya mapokeo.

ZIJUE AINA ZA WATUMISHI WA KANISA
1.     Watumishi wa kweli wakiitwa na MUNGU, hawarudi nyuma kwa kulichanganya NENO na uongo. Ni lazima MUNGU amtume yeye binafsi.

2.     Watumishi wa kimapokeo: Hawa ni watumishi ambao wamejiita au wametumwa na shetani au walimwacha MUNGU na bado wanahubiri kwa kupitia roho nyingine ya giza. Wengine huteuliwa na watu na siyo MUNGU na kaisomea hiyo kazi ya uchungaji. Nataka muelewe siyo mbaya kwenda bible college lakini je hiyo bible college haina mapokeo ya wanadamu? Mfano jiulizeni enyi dunia mnaompenda Mwenyezi MUNGU na mseme kweli je hizo shada (degree/PhD) anazozipata mtu halafu anakubatiza kwa kikombe au kwenye kisima, je atabisha kwamba hizo siyo PhD za kibinadamu? Jibu lipo wazi napenda muelewe, mimi sina mipaka katika injili ya YESU, nasema anachonielekeza hata mimi nilikuwa sijui elimu hii ila ndiyo kweli hata uombe, na umuulize MUNGU kuhusu elimu za uongo atakwambia siri zake, hizo ni za mpinga kristo, ni za kimapokeo. Na zaidi ukiwa mnafiki kwa YESU, yaani ukiona ukweli, hutasema ile kweli ili isimame imara bali utachukia kwa sababu tayari ulishakuwa mwana wa wanadamu na siyo mwana wa MUNGU, ila asiye mnafiki kwa YESU atatubu na kuachana na taratibu hizo na atamtukuza MUNGU kwa ajili ya uponyaji alioupata.

3.     Huduma kuwa na ma-partners, wanachaguliwa na kiongozi wa huduma kwa sababu ni watu wenye uwezo kifedha, eti hao ndio waliochaguliwa na MUNGU. Hayo ni mapokeo yake huyo mtumishi. Na zaidi ndani yake anakuwa analo pepo tamaa na uwizi na pepo la unyang’anyi, akiwa ni mwana wa shetani mwaminifu katika unyang’anyi.

4.     Mapokeo ya shetani ya kuwadai watu pesa makanisani, yaani kila muumini lazima alipe kiasi fulani cha pesa na asipo lipa mtu huyo akifa hawamziki. Msilipe, huo ni ushetani kabisa, YESU hajaleta mambo hayo, hayo ni mambo yao ya kitapeli. Huduma au kanisa likianza mtindo huo tayari linakuwa ni la kitapeli kwa sababu huu ni utapeli. Tafuta katika Biblia, hairuhusiwi kabisa, sasa hii imetokea wapi? Mwenye akili na aelewe.

5.    Kumwona mtumishi yeyote haupaswi ulipe pesa kwa secretary ndio upewe appointment, anatakiwa awahudumie kwa upendo, hivyo ndivyo watumishi wa YESU walivyo. Kanisa siyo hospitali,  yaani kumwona daktari lazima kwanza utoe pesa, hayo ni mambo ya kaisari, kaisari hamwangalii MUNGU na MUNGU haangalii ya Kaisari, na ndiyo maana YESU alisema ya Kaisari mpe Kaisari na ya MUNGU mpe MUNGU. Sasa kanisa limekuwa Kaisari? Jibu hapana na kama siyo basi usitegemee kukutana na MUNGU mahali ambapo yamefanyika mambo ya kikaisari.

Angalizo:

Yapo mapokeo mengi ila MUNGU akufunulie zaidi ili ushinde. Tubu, sema, BWANA YESU, naomba unisamehe dhambi zangu zote, uniandike jina langu katika kitabu chako cha uzima. Ulitoe jina langu katika kitabu cha mapokeo ya wanadamu, nahitaji kuwa mwana wa MUNGU na siyo mwana wa mapokeo ya wanadamu, nikijua kuwa ule mwisho mimi nitaenda mbinguni na siyo kwenye mapokeo ya wanadamu, nayafuta, najitenga nayo kwa jina la YESU. Amen.

NABII HEBRON WILSON KISAMO


USISAHAU KUSUBSCRIBE YOUTUBE CHANNEL
 YETU YA PROPHET HEBRON KWA KUBONYEZA LINK HII https://www.youtube.com/prophethebron?sub_confirmation=1 KUTAZAMA
 VIDEO ZAIDI