Pages

Saturday, May 19, 2018


YESU ALIMAANISHA NINI KWA KUSEMA, MBWA MWITU MJIEPUSHE NAO

BWANA YESU ASIFIWE. Katika Neno hili alilolisema YESU, “mjiepushe na mbwa mwitu”, MATHAYO 7:15. YESU hakumaanisha ni wale wanyama wa porini ambao wanaitwa “wild dogs” bali alimaanisha ni kiroho baada ya yeye kuondoka. Nitaelezea kwa ufupi kuhusu tabia za huyu mnyama kwa sababu nimepata bahati ya kusoma elimu ya wildlife na nimewaona kwa macho na kujua tabia zao vizuri. Huyu ni mbwa wa tofauti ni mkali kupita mbwa wanaotunzwa na wanadamu, wanaitwa mbwa mwitu kwa sababu wanadamu hawawezi kuwafuga. Nitaelezea kwa kifupi, wakiwa wanawinda mnyama hawa mbwa mwitu humkimbiza mnyama wakiwa katika kundi  (in group) na kila mbwa mwitu hung’ata sehemu ya mnyama wanayemkimbiza na muda wote mbwa mwitu hao wakiwa bado wanakimbia huendelea hivyo hivyo kung’ata na kula mpaka pale mnyama anapoanguka chini. Mnyama huyo anapoanguka hubakia na sehemu kidogo ya mwili wake au kwa maana nyingine hawa mbwa mwitu humla mnyama pasipo kumuua kwanza, bali wakiwa katika kundi humla mnyama huyo akiwa bado mzima mpaka pale atakapoishiwa nguvu na kuanguka chini na kufa, ni mbwa wakatili sana na kwa kingereza wanaitwa wild dogs.

Sasa kwa nini YESU alisema angalieni mbwa mwitu watakuja na kwa nini wasiwe hawa mbwa mwitu wa porini wakaja makanisani? Badala yake hawa mbwa mwitu wakawa ni watumishi wa kiroho katika injili, na kama ni mbwa mwitu wako katika injili basi uelewe wanawinda wana wa MUNGU wanaomtafuta au kumpenda YESU ili wauwawe kiroho na hata kutimia kimwili. Neno hili nafikiri ni watu wengi hawalijui maana yake na inawezekana hata unayesoma ujumbe huu pasipokujua au kwa kujua tayari umekuwa mbwa mwitu na siyo mchungaji na kama ni mbwa mwitu basi siyo mchungaji aliyeitwa na Mungu bali ni mchungaji jina tu. Ndio sababu YESU akasema kwa nje wamevaa ngozi ya kondoo ila ndani yao ni mbwa mwitu, maana yake kwa nje anaitwa au kuonekana ni mchungaji ila anayoyatenda na yaliyojaa ndani yake ni mbwa mwitu. Sasa kama unayotenda mambo ya tabia za mbwa mwitu, hapo inakuhusu kuitwa na YESU wewe ni mbwa mwitu wa kiroho. Ninaposema mbwa mwitu wa kiroho nina maana ni wale baadhi ya wachungaji au watumishi ambao kwa nje au kwa majina wanaonekana au kuitwa ni watumishi wa MUNGU ila ndani ya mioyo yao wana mipango tofauti na Roho Mtakatifu, haijalishi jina la YESU linatajwa au Biblia kusomwa. Kumbuka YESU alisema watatumia jina langu kuwateka hata wateule, yaani wale waliookoka, na ambao bado hawajaokoka na ambao wapo njiani kumpokea YESU wakazuiliwa kutokuokoka.

Kazi ya mbwa mwitu katika kanisa ni kuua kiroho au kuyaharibu yale ambayo YESU aliyaacha yafuatwe ili watu waweze kuurithi uzima wa milele na kwenda mbinguni. Shetani akaingiza roho mbaya ndani ya baadhi ya wachungaji waliomsaliti YESU na wale wengine waliojiita na wengine wale ambao wamezaliwa kiroho na shetani japo ni wanadamu, hivyo ile roho ya shetani ndiyo itendayo kazi, roho ya mbwa mwitu, roho ya kuua roho za wanadamu, roho ya kula pesa za waumini kwa kuwadai pesa za maombezi wakati neno linasema nimekupa bure, toa bure. Endapo mtumishi ataanza kuwatoza watu pesa, tayari yeye anaitwa ni mbwa mwitu na siyo mchungaji kwa sababu hili analolifanya siyo mapenzi ya MUNGU aliye Mbinguni, bali ni mapenzi ya baba yao ambaye ni joka kuu aliye kuzimu. Haijalishi anajua au hajui. MUNGU analiangalia Neno lake. Swali, je kutoza watu pesa ni la Mbinguni? Jibu siyo la Mbinguni, hivyo basi mchungaji anapofanya hivyo tayari yeye anaitwa mbwa mwitu na hata hao anao waongoza kiroho hawawezi kuwa kondoo wa YESU, bali watakuwa na wao ni watoto wa mbwa mwitu. Biblia inasema, jinsi alivyo mchungaji ndiyo taswira ya waumini wake, hivyo usipende kuwa mtoto wa mbwa mwitu wakati wewe unapenda kuwa kondoo wa YESU.

Nitaelezea kwa ufupi na ulimwengu wote uelewe hata na wayahudi kwa sababu baadhi mnapenda kwenda mbinguni, lakini tambua ya kwamba mbwa mwitu hakufikishi mbinguni bali anakuamgamiza kiroho na kukunyang’anya mali zako kwa kutumia jina la YESU au hata kukubatiza ubatizo ambao ni tofauti, ubatizo usiojulikana ulipotoka na kumfanya mtu apokee ubatizo wa uongo na kwa njia hiyo hupokea kibali cha kutengwa na YESU pasipo kujua. Ndiyo sababu YESU akasema ubatizwe ili uwe mwanafunzi wake. Sasa jiulize umeupokea ubatizo alioupokea YESU, ambaye yeye ndie njia? Basi endapo umepokea tofauti na ubatizo alioupokea YESU, yakupasa kujua kwamba katika ulimwengu wa roho upo katika njia ambayo siyo Yake, unatembea katika njia ambayo siyo yake, unatembea katika njia ya mpinga kristo, japo haupendi au unajua. YESU amenituma niwaeleze ili mbadilike, hiki ni kipindi cha neema, yeye anarudi na atawachukua wale wenye kibali chake au kiapo cha ubatizo wake.

NI JINSI GANI MCHUNGAJI ANAWEZA AKAGEUKA AKAWA MBWA MWITU
1.     Akianza kuwadai watu pesa za maombezi.

2.     Akibatiza tofauti na ubatizo aliobatizwa YESU wa maji mengi yanayotembea na yasiwe hata ni ya kisima au ubatizo wa maji ya kikombe au hata wa maji mengi yanayotembea halafu ukabatizwa kwa jina la mchungaji; mchungaji huyo mbele za YESU na mbingu anakuwa ni mbwa mwitu, iwe anajua au hajui kuwa hayo ni makosa, na anakuwa ameivunja amri ya MUNGU au kuipindua, soma Ufunuo 22: 18-19.

3.     Anapofanya maombezi ya kupanga kiwango fulani cha kutoa au hata kupanga viti maalum katika ibada au mtumishi anayetangaza kwamba atawawekea mikono wale tu watakao toa labda dola 1000, wao watapewa sehemu maalum ya kukaa, hivyo lipia mapema ili ukutane na MUNGU au muujiza wako. Nakueleza wewe uliyelipia na utakayoendelea kulipia bado hautakutana na MUNGU kabisa bali unajitolea sadaka kwa mashetani pasipo wewe kujua, ila huyo mchungaji anajua anachokifanya na mpaka afanye hivyo ameshakua sugu kabisa, amejawa na ujasiri wa shetani, hivyo unakuwa umekutana na mbwa mwitu na wamekula pesa zako au kukunyang’anya mali zako wakitumia jina la YESU. Ndugu kama ulishakutana na jambo kama hilo uelewe ulikwenda kwa mbwa mwitu na siyo mchungaji wa YESU, na zaidi unapotoa pesa katika ulimwengu wa roho ambao kiuhalisia ni wa giza, wanatumia mapepo na majini kukuharibia vitu vyako na matokeo yake wewe unajua ulitoa pesa ili ujibiwe na MUNGU lakini hauoni majibu, na hali inazidi kuwa mbaya, tambua ya kwamba mapepo mbwa mwitu yanaendelea kula vitu vyako ukiwa hai huku unatembea ila haujielewi na kama si Neema ya MUNGU ikakutana na wewe hautapona, utaangamia kabisa, kwa sababu picha halisi ya mtu kwenda Mbinguni inahusiana na uhusiano wake mzuri alionao na MUNGU wakati akiwa hai, ukiona uhusiano na MUNGU ni mbaya basi utaenda kwa wabaya na kama hutajitoa au kujitenga na kutoshirikiana kabisa na mbwa mwitu kiroho pamoja na ibada zao, basi unakuwa umefanana na mwana wa mbwa mwitu na wewe utafuatana nao siku ile ya mwisho.  Tafuta mahali ambapo yupo mchungaji wa kweli wa MUNGU na siyo mchungaji mbwa mwitu. Kama nilivyoelezea kuhusu tabia za mbwa mwitu (wild dogs) kimwili na kiroho wana tabia hizo hizo; za kuua kila kitu hata karama uliyonayo au vipaji au maono au mipango mizuri aliyokupangia mwenyezi MUNGU hapa ulimwenguni.

4.     Anapofanya harambee au minada ya masoko katika nyumba ya MUNGU, tendo hilo YESU alilikataa na aliwafukuza, soma Marko 11: 15-18. Sasa mbwa mwitu wa kiroho wamerejesha biashara katika nyumba za ibada na matokeo yake watu hawamwoni MUNGU bali ni mateso na dhiki tupu kwa sababu mbwa mwitu haleti baraka hata siku moja na wala haleti uzima bali huleta kifo cha kiroho tu. Watu wengi sasa katika ulimwengu wapo makanisani lakini wameshakufa kiroho, wapo wapo tu, wanakwenda kanisani kama vile mazoea tu au sheria hauoni mabadiliko yoyote, hiyo ni dalili hapo ulipo siyo sahihi kwako, ondoka pana ukame wa kiroho, hapo pana masika ya kiroho ya shetani.

Hata kudaiwa pesa ndipo ukamwone mchungaji ili akuombee sio sahihi, usitoe kwa sababu huyo anayekudai kwa kutumia jina la YESU katika moyo wake yupo pepo mbwa mwitu na hao ndio mbwa mwitu aliowasema YESU.

Mtumishi ambaye anawachagua watu na kuwaita partners wake na anawapa daraja la jina la kitu cha thamani sawa sawa na jinsi mtu anavyotoa kwa ajili ya huduma hiyo mfano gold, diamond (almasi), tanzanite na mengine mengi, uelewe huyo ndio aina ya hawa mbwa mwitu aliowasema YESU na mtawajuaje, mtawajua kwa matendo yao ya kuwatesa wanadamu kwa kuwatawala na elimu ya mapokeo ya shetani. Na zaidi mambo hayo hupewa baadhi ya watumishi wayafanye ili wafanikiwe kujenga ufalme wa shetani au mpinga kristo hapa duniani. Kwa njia ya kuiba kwa kisaikolojia. Nawaeleza wote hakuna baraka utapata kutoka mbinguni, kwa sababu huyo anayefanya hayo ndio mbwa mwitu wa kiroho anayewachagua kondoo wale walionona na kuwaacha wale kondoo waliokonda. Wenye uwezo kifedha ndio wanono na maskini ni kondoo waliokonda.

YESU alikuja kwa ajili ya watu wa jinsia zote. Hakuja kuangalia wenye mafanikio tu, watu wote ni wake na wala hana tabaka. Amenituma niwaeleze ili utakayependa utafunguka na uchukiaye ukweli utabakia kuangamia na kuteseka. Enyi watumishi wa jinsi hiyo, someni Biblia na maelekezo ya YESU, ameyakataza mambo hayo kabisa, ukiyakifuata tu inakuwa ni kumfuata mbwa mwitu. Na kama unamfuata mbwa mwitu basi unakuwa tayari ni mawindo yao na kukufanya kuwa umeshawindwa na kutekwa na shetani kupitia wao.

Kulazimisha au kuwaomba waumini walipie kiasi fulani kama sheria iliyopitishwa na kanisa na endapo muumini atashindwa kulipa hiyo pesa basi endapo atapata msiba au tatizo kanisa halitashughulika na yeye. Kitendo hicho kinafanya mchungaji huyo kuitwa mbwa mwitu na YESU kabisa kwa sababu hayo siyo ya Mbinguni. Kazi ya kanisa ni kuhubiri injili, watu waonyeshwe njia nzuri apendayo YESU na kumfuata YESU na siyo kufanya mambo ya kaisari kanisani au kutembelea waumini katika nyumba zao na kudai pesa. YESU hayupo hivyo, na ndiyo sababu alisema muwe makini naondoka naenda Mbinguni, mbwa mwitu watakuja na hata sasa wamejaa wakiwauma baadhi ya wakristo katika ulimwengu wote.

Kama ulipewa risiti baada ya kutoa sadaka yako au kupewa cheti cha shukrani (congratulations) eti ya kwamba umekuwa mtoaji mwaminifu basi uelewe huyo siyo mchungaji wa YESU bali huyo amekuwa tayari mbwa mwitu. Yapo mambo mengi ila nitaelezea machache kwa leo ili mpate kuwaelewa mbwa mwitu ambao YESU alisema, ili muwajue wakoje na mtawajuaje. Na vile vile uweze kujua utajilindaje nao ili usije ukang’atwa na mbwa mwitu wa kiroho. Najua hata wengi mnaosoma mmeelewa, zaidi na wengine mpo katika mabanda yao kwa sababu mwokozi YESU yeye anajenga kanisa na katika kanisa mambo hayo hayataki anaumia roho yake kwa sababu anampenda BABA yake, tena bila unafiki na je kwa nini mtumishi asimpende YESU bila unafiki mpaka unaamua kuwa jangili au mwizi wa kufoji Neno la MUNGU ukidanganya watu kwa kuchanganya na uongo kwa sababu hawalijui Neno.

Amenituma mimi Nabii Hebron niwaeleze yote hayo. Mpo wengi mnalia na mmekata tamaa na MUNGU kwa sababu mbwa mwitu wamewang’ata kiroho mmebakia hoi. Sasa mtapona mtakapoachana nao mje kwake YESU wa kweli na Yeye atawaweka huru. Mbwa mwitu ndio hao watumishi ambao wanalitumia jina la YESU kufanyia biashara. Mtu mmoja alikuja kushtaki kwangu ana matatizo mengi, alienda aombewe lakini matatizo yapo pale pale. Na kuna siku mmoja akawa anasikiliza redio, mtumishi mmoja akatoa namba zake mwenye kuhitaji msaada zaidi ampigie, na yeye kijana akafanya hivyo akamweleza tatizo lake huyo mchungaji naye akasema MUNGU amesema tatizo lake ni kubwa sana hivyo atume sadaka kubwa, kijana akaogopa akachanganyikiwa akamwambia mimi sina sadaka kubwa, mchungaji akamuuliza anayo ngapi, kijana akamwambia ninayo TSh. 20,000/= akamwabia hiyo ni ndogo kijana akaomba apunguziwe (bargain) sadaka ya kutoa (jamani hii ni aibu, mchungaji ana bargain sadaka ya mtu), akamwambia MUNGU anataka utoe TSh. 60,000/=, kijana akamwambia sina kiasi hicho akiamini MUNGU anataka, akaongeza ikafika TSh. 30,000/= akampigia mchungaji, mchungaji akasema ni ndogo akakata simu. Sasa cha kushangaza baada ya kijana kukatiwa simu na yeye akaamua kuwa kimya, baada ya muda mchungaji akampigia simu kijana akamwambia haya tuma sasa hiyo TSh. 30,000/= kijana akajibu situmi tena, MUNGU gani huyu kigeugeu nilimpa TSh. 20,000/= akakataa, nikampa TSh. 30,000/= akakataa, akamwambia sitaki situmi tena, wewe siyo mtumishi wa MUNGU. Huu ni ushuhuda mfupi zipo shuhuda nyingi za jinsi hiyo, ingia katika website yangu www.prophethebron.or.tz katika link ya YouTube utayaona mengi na utaujua ukweli zaidi. Mwisho kijana alikuja nikamwombea akapona na alipopona akatoa ushuhuda akimfurahia MUNGU aliyemponya bila malipo yoyote. Sasa unaona, kijana huyu alikutana na mbwa mwitu na siyo mchungaji na labda hata na wewe umeshakutana nao, nakupa pole katika jina la YESU ila nakuombea uwekwe huru na usitumikishwe wala kutapeliwa.

Ukisoma Neno la MUNGU linasema mtumishi wangu unapopata tatizo usijisumbue wewe rudi kwangu niombe nitafanya.  Sasa ni aibu tupu kama kuna sehemu roho za ukoma au omba omba ya mahitaji zimejaa katika baadhi ya makanisa na kama hizo roho za shida ndizo zipo, sasa hauoni YESU hayupo hapo. YESU aliwaweka huru watu wote wenye mateso,  shida na vifungo mbali mbali bila malipo yoyote.

Angalizo:
Kwa ufupi, uwatumie ujumbe huu na wengine wakatae kuongozwa na mbwa mwitu au mpinga kristo, kwa sababu hao ndio mbwa mwitu aliowasema YESU. Najua maelfu hamkuelewa maana ya fumbo hili, nina amini kwa sasa mmelijua na baadhi ya watumishi wengi baba zao wa kiroho pasipo kujua na wengine wakijua wamewaingiza katika mtego huu, sasa tubu, ili uwe kondoo mzuri wa YESU na utengwe na kundi la mbwa mwitu wa kiroho. Sema najitenga na mbwa mwitu wote wa kiroho katika jina la YESU. Amen.

NABII HEBRON.

USISAHAU KUSUBSCRIBE YOUTUBE CHANNEL
 YETU YA PROPHET HEBRON KWA KUBONYEZA LINK HII https://www.youtube.com/prophethebron?sub_confirmation=1 KUTAZAMA
 VIDEO ZAIDI